umojannguvu.blogspot.com

Tuesday 8 September 2015

Bulembo aonya udini na ukabila




MWENYEKITI wa Taifa wa Jumuiya ya Wazazi ya CCM, Abdallah Bulembo, ameonya juu ya siasa za udini na ukabila kwenye kampeni na kuitaka Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), kuchukua hatua dhidi ya mgombea urais wa Chadema, Edward Lowassa.

Alisema hayo jana kwa nyakati tofauti kwenye mikutano ya kampeni ya mgombea urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), Dk John Magufuli.

Alisema hayo katika wilaya za Mvomero mkoa wa Morogoro na Kilindi mkoani Tanga. Bulembo ambaye ni sehemu ya timu ya kampeni ya mgombea huyo wa Urais alisema: “Hili haliwezi kuvumiliwa. Wahusika wachukuliwe hatua.” Pia, alishauri waangalizi wa kimataifa wa uchaguzi mkuu wa Tanzania, utakaofanyika Oktoba 25 mwaka huu kuliweka katika kumbukumbu zao suala kuingiza udini katika kampeni.
Kwa upande wake, akihutubia katika maeneo mbalimbali ya wilaya hizo za Mvomero na Kilindi, Dk Magufuli aliwataka Watanzania kuwakataa wanasiasa, wanaojaribu kusaka madarakani kwa misingi ya dini na ukabila.

Alisema kwa asili, Watanzania ni wamoja, hivyo hawapaswi kukubali kurubuniwa na wanasiasa wanaojaribu kutumia kila njia kuhakikisha wanatimiza kiu ya kupata `ukubwa’.
“Watanzania ni wamoja, kamwe wasiwakubali kurubuniwa na pia wasimkumbatie yeyote anayefanya siasa zenye lengo la kuwagawa iwe kwa udini au ukabila…hawa watatufikisha pabaya,” alisisitiza Dk Magufuli.

Kauli hizo za Bulembo na Magufuli ambaye pia ni Waziri wa Ujenzi, zimekuja baada ya kuwapo kwa taarifa kuwa mgombea urais wa Chadema, Edward Lowassa juzi Jumapili kujipigia debe kanisani kwamba yeye anastahili kuwa Rais wa Tanzania kwa sababu ni Mkristo wa madhehebu ya Kilutheri, ambalo halijawahi kutoa Rais tangu taifa hili lilipoundwa.

Lowassa kanisani
Lowassa alidaiwa kuyasema hayo akiwa katika Kanisa la Kiinjilili la Kilutheri (KKKT ) la Tabora mjini juzi Jumapili.
“Naomba mniombee, mniombee kwelikweli. Nyie Walutheri mna sababu ya kuomba zaidi. Kwa sababu tangu nchi hii iumbwe haijapata kutoa Rais Mlutheri. Mwalimu Nyerere alikuwa Mkatoliki, Rais (Benjamin) Mkapa alikuwa Mkatoliki. “Sasa nadhani Mungu atatuongoza ili nasi tuweze kuipata nafasi hiyo. Kwa hiyo naomba mniombee sana” alisema.

Kwa mujibu wa picha za video, zilizosambazwa katika mitandao mbalimbali ya kijamii pamoja na watumiaji wa simu za mkononi zenye mtandao wa WhatsAPP, Lowassa alitumia sekunde 23 kueleza maneno yake hayo na baadaye alisikika akianza kuimba nyimbo.

Picha hiyo ya video inaonekana kupigwa na mmoja wa waumini, waliokuwepo kanisani wakati Lowassa akizungumza. Video hiyo iliyosambazwa na mtu asiyejulikana, inamwonyesha Lowassa akiwa amevalia shati lake la rangi ya bluu na akizungumza kwa kutabasamu mbele ya waumini wa kanisa hilo.
Hotuba hiyo fupi ya Lowassa iliyomalizwa kwa pambio, haikutaja pia kwamba zaidi ya Nyerere na Mkapa, Tanzania pia imewahi kuwa na marais wengine wasio Wakristo; Ali Hassan Mwinyi na Jakaya Kikwete.

Mshindani mkuu wa Lowassa katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka huu, Dk John Magufuli wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) si Mlutheri kama Lowassa, hivyo mgombea huyo wa vyama vinne vinavyounda Ukawa, alikuwa akitumia dhehebu lake kujipatia faida dhidi ya mpinzani wake huyo. Mbali na Chadema, vyama vingine vinavyounda Ukawa ni CUF, NCCR-Mageuzi na NLD.
Makamba anena

Katibu Mkuu za zamani wa CCM, Yusuf Makamba, alisema mara nyingi wanasiasa wanaoishiwa mbinu, hukimbilia kuwagawa watu kwa misingi ya udini.
Kwa mujibu wa sheria za uchaguzi hapa nchini, wagombea wa nafasi zote za kisiasa hawaruhusiwi kufanya kampeni katika nyumba za ibada au kufanya siasa, zinazochochea ubaguzi wa aina yoyote.

Taarifa ya Tume ya Uchaguzi
Wakati huohuo, Mwenyekiti Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), Jaji mstaafu Damian Lubuva amevitaka vyama vyote vinavyoshiriki katika uchaguzi mkuu, kuzingatia maadili, huku akisisitiza Tume isilazimishwe kuchukua hatua za kutoa adhabu kwa vyama na wagombea.

Badala yake, amesisitiza kuwa busara itumike katika mikutano yote ya kampeni, zinazotarajiwa kufikia ukingoni Oktoba 24 mwaka huu, baada ya kuwa zimezinduliwa rasmi Agosti 22.
Katika taarifa yake kwa vyombo vya habari, jijini Dar es Salaam jana, Jaji Lubuva alisema licha ya kuwa kampeni zimeanza katika sehemu nyingi nchini, Tume imeanza kupokea malalamiko kadhaa, hivyo kuvitaka vyama na wagombea kuwa makini katika kuzingatia Sheria, Katiba na Maadili ya Uchaguzi wa Rais, Wabunge na Madiwani ya mwaka 2015.

Alisema; “Tangu Kampeni zianze, nafurahi kusema kwa niaba ya Tume kuwa kwa ujumla, Kampeni zimeenda vizuri. Karibu mikutano yote imefanyika katika hali ya utulivu na amani. Hatujapata taarifa ya mkutano wa kampeni ambao umevurugwa kwa fujo zozote. Kwa hilo napongeza vyama vyote vya siasa. “Hata hivyo, kutokana na mikutano hiyo nchini ya kampeni ngazi ya urais, ubunge na udiwani yamejitokeza mambo ambayo ni kinyume kabisa na Mwongozo wa Maadili ya Uchaguzi wa Rais, Wabunge na Madiwani wa mwaka 2015 uliotiwa saini na Vyama vyote vya Siasa tarehe 27 Julai, 2015.”

Alieleza kuwa baadhi ya mambo yaliyojitokeza katika kampeni hizo ni kutozingatia muda wa kumaliza mikutano ya kampeni, kubandika mabango ya kampeni, matangazo au mchoro wowote kwenye maeneo yasiyoruhusiwa au bila idhini ya wahusika, kuchafua, kubandua au kuharibu matangazo au picha za kampeni za vyama vingine na pia kuwapo kwa matumizi ya lugha zisizo za staha.

Kutokana na kuibuka kwa mambo hayo, alisema viongozi wa vyama vya siasa na wagombea wana wajibu wa kisheria wa kuyaheshimu, kuyasimamia na kuyatekeleza maadili ya mchakato wa uchaguzi, huku wakiwajibika pia kuwaelimisha, kuwahamasisha na kuwasisitiza wanachama wao kutekeleza Sheria ya Uchaguzi.
Kinyume cha hapo, alisema adhabu za ukiukwaji wa maadili ya uchaguzi, zinaweza kutolewa hivyo kuweza kusababisha chama au mgombea kuathirika kwa namna moja ama nyingine, ikiwa ni pamoja na chama au mgombea kusimamishwa kuendelea kufanya kampeni.

Adhabu nyingine imeelezwa kuwa chama au mgombea anaweza kuzuiliwa kutumia vyombo vya habari, na wakati mwingine chama au mgombea anaweza kulipishwa faini ya hadi Sh milioni moja.
“Katika kipindi hiki cha kampeni, Chama au Mgombea akipewa mojawapo ya adhabu hiyo, kunaweza kuathiri kampeni zake za kuelekea uchaguzi wa Rais, Wabunge au Madiwani,” alisema Jaji Lubuva.



 

0 comments:

Post a Comment

Drop Down MenusCSS Drop Down MenuPure CSS Dropdown Menu

CHAT BOX

Post zilizo tumwa

Recent Posts Widget

Tangaza Biashara yako mtandaoni

TANGAZA BIASHARA NAMI HAPA KWA BEI NAFUU KABISA

Unaweza kutangaza biashara yako sasa na hlmservice pia uta pata kujua mambo mengi ambayo mbali na biashara yako unaweza ukatengeneza pesa kwa namna moja ama nyingine kama jinsi nilivo elezea katika Makala za nyuma hapo

Wafanya biashara wengi wanatumia mda mwingi namna gani ya kukuza biashara zao ,Ili uweze kufanikiwa kwa kiasi kikubwa unahitaji kuitangaza biashara yako ili kuwa na mtandao mkubwa na wateja wako ,ni vyema ukatangaza biashara yako katika mitandao ili bidhaa zako zijulikane kwa haraka na upesi .

Pia wewe mfanya biashara ukiitaji kuwa na blog yako wasiliana nami kwa mawasiliano hapo chini , bei ni nafuu kabisa

Pia ukiitaji kuitangaza biashara yako kupitia blog yangu bei ni ndogo kabisa huu ni wakati wako wewe mfanya biashara

+255758061575 & +255684860817

henrylameck@gmail.com

henrylameck90@yahoo.com

Tukuyu Tour & Safari

Vadacom Ni Zaidi

Tembelea g2g.fm upate movie Kali

Tembelea g2g.fm upate movie Kali

Kilimo Kwanza

Hlm servise

Latest movie

Movies

Computer books

Computer books