umojannguvu.blogspot.com

Friday 21 August 2015

Tanapa yaanzisha kampeni kuhamasisha utalii wa ndani




SEKTA ya Utalii ni muhimu katika ukuaji wa uchumi nchini kwa kuwa inachangia kuliingizia Taifa fedha za kigeni.

Utalii unategemea uwepo wa maliasili na vivutio ili kuwavutia wageni kuja kutembea kufurahia ama kujifunza mambo mbalimbali yanayopatikana Tanzania. Kwa kutambua umuhimu wa sekta ya utalii, mwandishi wa makala haya amefanya mahojiano na Mkurugenzi Msaidizi Idara ya Utalii, Uzeeli Kiangi na kueleza hali ya utalii nchini na mchango wake katika ukuaji wa uchumi wa Tanzania.

Kiangi anasema Tanzania ni moja ya nchi chache duniani zilizojaliwa kuwa na vivutio vingi vya utalii ikiwemo mbuga za wanyama, mito na mabonde ya kuvutia pamoja na maajabu mengine. Anasema Tanzania ni nchi pekee ambayo zaidi ya asilimia 25 ya nchi kavu ni eneo lenye misitu ya hifadhi za wanyamapori pamoja na maeneo ya mapori ya akiba yaliyotengwa na serikali.

Kiongozi huyo anasema, moja ya vivutio vikubwa ni hifadhi ya wanyama ya Serengeti, Bonde la Ngorongoro , Ziwa Manyara pamoja na mlima mrefu kuliko yote barani Afrika, Mlima Kilimanjaro. Vivutio vingine ni pamoja na hifadhi za wanyama za Mikumi, Ruaha na Selous ambazo kila moja ina wanyama au miti ambayo ni adimu na inapatikana Tanzania pekee. Kiangi anasema utalii umegawanyika katika sehemu kuu mbili ambazo ni utalii wa ndani na utalii wa nje.

Utalii wa ndani ni ule ambao Watanzania wanatembelea maeneo tofauti na pale wanapoishi au kutembelea hifadhi na vivutio vingine vinavyopatikana nchini. Utalii huu hujumuisha mapumziko ya familia hasa wakati wa likizo katika moja ya hifadhi za taifa au maeneo mengine ya utalii yanayopatikana ndani ya nchi pamoja na utalii wa kimasomo. Utalii wa nje unahusisha watalii ambao wanasafiri kutoka nchi mbalimbali na kuja Tanzania kwa ajili ya kupumzika wakati wa likizo, utalii wa masomo na kufanya tafiti pamoja utalii wa kuja kujionea wanyama na vitu vingine visivyopatikana katika maeneo yao.

Kwa mujibu wa Kiangi, watalii wanaotoka nje ya nchi kuja Tanzania ni wengi kuliko wale wa ndani. Anasema watalii wa kutoka nje ya Tanzania wamekuwa wakiongezeka mwaka hadi mwaka kutoka watalii 295,312 mwaka 1995 hadi kufikia watalii 1,140,156 mwaka 2014. Ukuaji wa utalii hadi kufikia mwaka jana 2014, umesaidia kuongeza kasi ya ukuaji wa uchumi na kusaidia juhudi za serikali katika kuleta maendeleo kwa wananchi.

Ongezeko hili la watalii limesaidia kuongeza upatikanaji wa fedha za kigeni kutoka dola milioni 259.44 mwaka 1995 sawa na Sh milioni 155,663 hadi kufikia dola milioni 2,006.32 sawa na Sh milioni 3,316,647.59 mwaka 2014. Kiangi anasema, watalii wengi hufika nchini kwa kutumia zaidi usafiri wa anga. Mwaka jana watalii 636,107 walitumia usafiri huo na watalii 439,421 walifika kwa kutumia usafiri wa barabara.

Aina nyingine ya usafiri inayotumika ni usafiri wa maji. Mwaka jana watalii 59,999 waliingia nchini kwa kutumia usafiri huo na wengine wapatao 4,629 waliingia kwa kutumia usafiri wa reli. Anasema, watalii wengi hufika nchini kwa sababu ili kupumzika wakati wa likizo kazini. Kwa mujibu wa Kiangi, mwaka 2014 watalii 920,028 walifika kwa ajili ya mapumziko. Mwaka jana watalii 85,818 wanafika kwa ajili ya kutembelea marafiki, ndugu na jamaa zao wa karibu, 68,341 wanafika kwa ajili ya shughuli za kibiashara na mafunzo ya kitaalamu.

Pamoja na ukuaji huo wa utalii, Kiangi anasema bado utalii wa ndani haujawa na hamasa kubwa kama ulivyo utalii wa nje kutokana na kuwepo na idadi ndogo ya Watanzania wanaojihusisha na utalii wa kutembelea vivutio vilivyopo nchini. Kiangi anasema, utalii wa ndani unakua taratibu kwa kuwa wananchi wengi wanaogopa gharama kubwa za chakula, malazi na usafiri.

Anasema, serikali itaanzisha usafiri maalum pamoja na kuwekeza kwenye hoteli zitakazotoa huduma nafuu ya chakula na malazi katika hifadhi za taifa ili kukuza utalii wa ndani. Kiangi anasema, serikali itawekeza kwenye hoteli zitakazotoa huduma ya chakula kwa bei ndogo ambazo kila mwananchi ataweza kuimudu. Katika juhudi za kuhakikisha kuwa utalii wa ndani unakua, Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA) hivi karibuni linatoa wito kwa wananchi kutembelea hifadhi za taifa ili waweze kunufaika kwa kujionea vivutio pamoja na kupata zawadi maalumu.

Kampeni ya uhamasishaji utalii wa ndani ni moja ya hatua muafaka zinazochukuliwa na serikali kwa kushirikiana na wadau ili kuongeza idadi ya Watanzania wanaotembelea hifadhi za taifa na kuongeza mapato kupitia utalii. Mkurugenzi wa Utalii na Masoko kutoka TANAPA, Ibrahim Mussa anasema, utalii wa ndani umeongezeka lakini kwa idadi ndogo ukilinganisha na watalii kutoka nje ya nchi.

Mussa anasema, utalii wa ndani ni rasilimali kubwa lakini bado Watanzania wana mwitikio mdogo katika jambo hilo. Anasema, TANAPA imeanzisha kampeni ya kuhamasisha wananchi kutembelea hifadhi za taifa kwa kipindi cha miezi sita kuanzia Julai hadi Desemba mwaka huu. Mussa anasema, kutakuwa na usafiri kuwapeleka wananchi hadi hifadhi za taifa ikiwa ni njia mojawapo ya kupunguza gharama pamoja na kutoa huduma ya chakula na malazi kwa bei nafuu kwenye hoteli za kitanzania zijulikanazo kama Mabanda lakini zenye huduma nzuri na nafuu.

Anasema, huduma hiyo ya mabanda itawawezesha wananchi kupata huduma ya malazi kwa bei ya chini kuanzia Sh 15,000 hadi 80,000 kitu ambacho wananchi wengi wanaweza kumudu. Mussa anasema, mwaka jana idadi ya watalii wa ndani imeongezeka hadi kufikia laki nne na nusu hivyo kuonesha kuwa endapo juhudi zaidi zitafanyika kuhamasisha wananchi kutembelea hifadhi za taifa, wananchi wengi zaidi wataenda kutalii.

Ili kuhifadhi vivutio vilivyopo, Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kushirikiana na wadau ikiwemo Wakala wa Taifa wa Misitu watasaidia kulinda na kurejesha madhari rafiki kwa ajili ya ukuaji wa utalii. Wakala hiyo imesaidia upandaji wa miti kwenye eneo la hekta 40,000 katika mashamba 18 nchi nzima na kufikisha jumla ya hekta 96,500 zilizopandwa nchini na kupunguza hali ya jangwa iliyokuwa ikiongezeka kila mwaka.

Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Taifa wa Misitu, Juma Mgoo anasema, wamepata mafanikio ikiwemo kufanikisha upandaji wa miti na kuokoa baadhi ya misitu iliyokuwa hatarini kutoweka. Mgoo anasema, wamefanikisha kuingiza Sh bilioni 85.3 kwenye pato la taifa kwa mwaka 2014/2015 ikiwa ni ongezeko kubwa ukilinganisha na Sh bilioni 39 walizochangia kwenye bajeti ya mwaka 2010.

Anasema, wameweza kupima na kuweka mipaka ya misitu ya taifa 102 ambayo ni sawa na asilimia 25 ya misitu yote 455 ya hifadhi iliyopo nchini. Mgoo anasema wanajivunia kuona utalii unazidi kukua na hivyo ni wajibu wa wananchi kuhifadhi na kutunza misitu ili iweze kusaidia kuvutia watalii pamoja na kuongeza pato la taifa.

Kiangi anasema, ujangili ni miongoni mwa mambo yanayoathiri sekta ya utalii na kwamba, madhara yake hayawezi kuonekana moja kwa moja hivi sasa. Kwa mujibu wa Kiangi, madhara ya uovu huo yataanza kuonekana baadaye hivyo ni wajibu wa kila mtu kuhakikisha analinda rasilimali za utalii zisipotee. Anasema jukumu la kulinda na kuhifadhi rasilimali za utalii na nchi kwa ujumla si la serikali peke yake.

 


0 comments:

Post a Comment

Drop Down MenusCSS Drop Down MenuPure CSS Dropdown Menu

CHAT BOX

Post zilizo tumwa

Recent Posts Widget

Tangaza Biashara yako mtandaoni

TANGAZA BIASHARA NAMI HAPA KWA BEI NAFUU KABISA

Unaweza kutangaza biashara yako sasa na hlmservice pia uta pata kujua mambo mengi ambayo mbali na biashara yako unaweza ukatengeneza pesa kwa namna moja ama nyingine kama jinsi nilivo elezea katika Makala za nyuma hapo

Wafanya biashara wengi wanatumia mda mwingi namna gani ya kukuza biashara zao ,Ili uweze kufanikiwa kwa kiasi kikubwa unahitaji kuitangaza biashara yako ili kuwa na mtandao mkubwa na wateja wako ,ni vyema ukatangaza biashara yako katika mitandao ili bidhaa zako zijulikane kwa haraka na upesi .

Pia wewe mfanya biashara ukiitaji kuwa na blog yako wasiliana nami kwa mawasiliano hapo chini , bei ni nafuu kabisa

Pia ukiitaji kuitangaza biashara yako kupitia blog yangu bei ni ndogo kabisa huu ni wakati wako wewe mfanya biashara

+255758061575 & +255684860817

henrylameck@gmail.com

henrylameck90@yahoo.com

Tukuyu Tour & Safari

Vadacom Ni Zaidi

Tembelea g2g.fm upate movie Kali

Tembelea g2g.fm upate movie Kali

Kilimo Kwanza

Hlm servise

Latest movie

Movies

Computer books

Computer books