umojannguvu.blogspot.com

Friday 21 August 2015

Teknolojia inavyoweza kudhibiti wizi wa simu, kurahisisha usafiri





UTAFITI na ubunifu vina nafasi kubwa katika kulinufaisha taifa, hasa ikizingatiwa kuwa hakuna nchi duniani inayoendelea bila kuzingatia ubunifu hasa kwenye masuala ya sayansi na teknolojia.

Tume ya Sayansi na Teknolojia (Costech) iliyopo chini ya Wizara ya Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia kwa kushirikiana na wahisani wamejikita katika kusaidia vijana walioonesha uwezo wa kubuni miradi ya maendeleo. Kituo cha Kuendeleza Teknolojia ya Habari na Mawasiliano kiitwacho DTBi cha tume hiyo ni msaada mkubwa kwa vijana wabunifu katika tehama.

Mkuu wa Utawala na Fedha wa kituo hicho, Makange Mramba anasema, lengo la kuanzisha kituo hicho ni kusaidia vijana wajasiriamali wa Tehama wenye ubunifu wa aina mbalimbali kuanzisha kampuni zao na wenye kampuni kusaidiwa ili zikue na kuchangia katika pato la taifa.

“DTBi tunawasaidia vijana waanzishe kampuni na wale ambao tayari wanazo basi kampuni zao ziweze kukua waweze kuchangia pato la Serikali kwa maana ya kulipa kodi na pia waweze kuajiri wenzao na pia kutoa ufumbuzi wa matatizo ambayo yanazikabili sekta zetu mbalimbali kama kilimo, madini, afya na nyinginezo,” anasema Mramba. Anasema katika kufanya hivyo, wizara kwa kushirikiana na wadhamini walikubaliana kianzishwe kituo chini ya mwavuli wa Costech Juni 2011.

Mramba anasema, baada ya kuanzishwa kituo hicho, kazi ya kwanza ilikuwa ni kuelimisha wajasiriamali kujitokeza wakiwemo waliokuwa vyuoni wakitengeneza programu lakini wanakumbana na changamoto mbalimbali ikiwa ni pamoja na upatikanaji wa mitaji, eneo la kufanyia kazi na pia elimu ya ujasiriamali. Anasema DTBi wana mfumo wa kutatua matatizo ya wajasiriamali wabunifu katika hatua ya mwanzo kwa kuwaunganisha na mitaji, kuwatambulisha sokoni na kuwapa ushauri kwa kuwa ni vijana wadogo wanaohitaji malezi na msaada wa kiteknolojia.

“Wengine wanahitaji msaada wa kiteknolojia, anaweza kuwa anajua jambo fulani lakini kuna ujuzi ambao hana ili atimize jambo analotaka kufanya kwa hiyo sisi tunawaunganisha na wataalamu ili waweze kusaidiwa kukamilisha jambo lao na wengine wanakuja na mawazo mazuri lakini wao sio wanateknolojia kwa hiyo tunawaundia timu ya wataalamu,” anasema Mramba.

Anasema kituo hicho kimeweza kujiimarisha na sasa watu wanakifahamu vizuri na kuna vijana waliojengwa na kituo hicho akitolea mfano wa MaxMalipo. “Ukinunua umeme, muda wa maongezi, ukilipia leseni ya gari kulipia malipo yoyote kwa kupitia MaxiMalipo unatumia huduma inayotokana na zao letu, tunda jingine ni Day One ambaye ametengeneza mfumo unaotumika na halmashauri mbalimbali kukusanya kodi,” anasema Mramba.

Anasema vijana wanakaa katika kituo hicho wakifundishwa biashara na pia teknolojia kwa miaka mitatu na baada ya hapo wanakuwa wameshakomaa, wanajitegemea huku wakiendelea kupokea ushauri. Mramba anasema, Day One imetoa msaada mkubwa katika kuwatambua walipa kodi na kuwaingiza katika mfumo wa malipo katika halmashauri 15 zikiwemo za Temeke, Arusha na Moshi. Anasema, kampuni hizo pia zimeweza kuzalisha nafasi za ajira kwa vijana waliokuwa wakihangaika mtaani.

Mramba anasema, kuna vijana wanatoka vyuoni moja kwa moja nao wanakubaliwa kujiunga kwenye kituo hicho na anatoa mfano wa kijana aliyeweza kutengeneza mfumo unaosaidia katika tatizo la wizi wa simu. Kijana huyo hivi karibuni ataingia mkataba na kampuni ya simu za mkononi ili mfumo huo uanze kutumika. Mfumo huo ni wa kulinda simu za mkononi za smart phone.

“Imekuwa ni vigumu sana unapoibiwa simu kupata taarifa zao zilizokuwa ndani ya simu lakini mfumo huo una uwezo wa baada ya kuibiwa simu, ukipata simu nyingine unaita taarifa zako zote zinakuja. “Baada ya kuibiwa simu yako, ukishapata simu nyingine unaingiza namba ya siri basi unaita taarifa zako zote zinakuja, ikiwa ni pamoja na namba za simu na picha.

Mfumo huu hivi karibuni utakuwa sokoni,”anasema Mramba. Anasema mfumo una uboreshwaji wa vitu ambavyo havipatikani katika mifumo mingine ya aina hiyo na kwamba, unaweza kuendelea kumfatilia mtu aliyechukua simu hiyo, kumtumia ujumbe mara kwa mara na pia hatakuwa na uwezo wa kuitumia wala kuifuta (flash) vitu vilivyopo kwenye simu hivyo atalazimika kuirudisha.

Mramba anasema, pia vijana walioko katika kituo hicho wameweza kutengeneza mfumo wenye uwezo wa kufuatilia, kwa mfano, mmiliki wa pikipiki za biashara maarufu kwa jina la bodaboda anaweza kutumia simu yake na pia unaweza kuizima boda boda hiyo kama anaona inaelekea sehemu ambayo huielewi. Kwa mujibu wa Mramba, kuna programu nyingine inayoweza kusaidia mtu kuona teksi iliyoko jirani na alipo kama anahitaji huduma hiyo hivyo badala ya kumpigia dereva aliye mbali na hapo atamwita aliye karibu.

“Programu hii pia itakuonesha teksi inayopita karibu na wewe namba yake ya simu, historia ya teksi hiyo pamoja na maelezo ya dereva husika... unaweza kuona kama imewahi kupata ajali au la, uzoefu wa dereva, na hii yote ni kwa kutumia simu yako ya mkononi,” anasema Mramba. Programu hiyo itaunganisha mfumo wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) pamoja na taarifa za Jeshi la Polisi na Kikosi cha Usalama Barabarani kwa ajili ya kupata taarifa na kuziunganisha kwa programu hiyo ambayo iko katika hatua ya kuiendeleza.

Anasema lengo la DTBi ni kutumia mfumo wa Tehama kutatua matatizo ya watu ambayo hadi sasa hayana suluhisho. “Sasa tunaandaa pia programu ya kuangalia televisheni kupitia simu ya mkononi ambazo ni smart phone, inaweza kukamata vituo vyote vya televisheni ukiwa popote huna haja ya kukimbia nyumbani kuangalia taarifa ya habari au kipindi chochote,” anasema Mramba.

Mramba anasema kituo hicho kinatafuta uwezekano wa kupanua wigo wa huduma ili kuwanufaisha watu wengi zaidi kwa kuwapata wabunifu wengine ambao wako katika mikoa mingine. Kwa sasa kituo hicho kinachukua vijana kutoka vyuo vikuu kadhaa ikiwa ni pamoja na Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM). Mramba anasema kituo hicho kinakabiliwa na changamoto ikiwa ni pamoja na wajasiriamali kutokuwa na mwamko wa kutumia fursa kama hizo.

“Wengine wanahangaika huko pembeni, pamoja na matangazo tunayotoa lakini hawajitokezi inabidi tuwatafute,” anasema Mramba. Anasema vijana wengi hawana mwamko wa kuwa wajasiriamali, wengi wao wanakimbilia kutafuta kazi baada ya kumaliza masomo yao badala ya kufikiria kujiajiri. “Hata wale wanaoweza kuwa wabunifu wazuri sana na kusaidia nchi wanakimbilia kupata ajira ambazo hazipo,”anasema Mramba.

Anataja changamoto nyingine kuwa ni kuingiza sokoni utaalamu walioubuni kwa sababu imeshajengeka imani kwamba teknolojia lazima itoke katika nchi zilizoendelea. Mramba anasema, bado watu hawaamini kwamba watu wanaowafahamu wanaweza kuja na jambo linaloweza kusaidia dunia. Kwa mujibu wa Mramba, mitaji ni moja ya changamoto kwa kuwa taasisi nyingi za fedha ikiwa ni pamoja na benki hawatoi mikopo kwa wabunifu hao kutokana na asili ya kazi zao ambazo zinachukua muda mrefu kuanza kurudisha fedha.

“Teknolojia zetu ukiwekeza mwaka huu unatarajia kuanza kuvuna baada ya miaka mitatu au minne, afanyie majaribio, apeleke sokoni ikafanyiwe majaribio na kukubaliwa na kuingia sokoni hii inachukua muda mrefu kwa hiyo huwezi kumpa mkopo ukamwambia aanze kulipa mwezi ujao,” anasema. Mramba anasema, unahitajika mfumo wa kuwatambua wabunifu hao ili wapewe muda wa kutosha kuanza kupata faida na kurejesha mkopo.

Anasema, Serikali pia inapaswa kutoa nafasi kwa wabunifu wanapokuja na teknolojia waweze kujaribu kwenye taasisi za serikalini au kwingineko inakohitajika. Mramba anasema, sheria na taratibu za sasa haziwaruhusu wabunifu kufanya hivyo.

0 comments:

Post a Comment

Drop Down MenusCSS Drop Down MenuPure CSS Dropdown Menu

CHAT BOX

Post zilizo tumwa

Recent Posts Widget

Tangaza Biashara yako mtandaoni

TANGAZA BIASHARA NAMI HAPA KWA BEI NAFUU KABISA

Unaweza kutangaza biashara yako sasa na hlmservice pia uta pata kujua mambo mengi ambayo mbali na biashara yako unaweza ukatengeneza pesa kwa namna moja ama nyingine kama jinsi nilivo elezea katika Makala za nyuma hapo

Wafanya biashara wengi wanatumia mda mwingi namna gani ya kukuza biashara zao ,Ili uweze kufanikiwa kwa kiasi kikubwa unahitaji kuitangaza biashara yako ili kuwa na mtandao mkubwa na wateja wako ,ni vyema ukatangaza biashara yako katika mitandao ili bidhaa zako zijulikane kwa haraka na upesi .

Pia wewe mfanya biashara ukiitaji kuwa na blog yako wasiliana nami kwa mawasiliano hapo chini , bei ni nafuu kabisa

Pia ukiitaji kuitangaza biashara yako kupitia blog yangu bei ni ndogo kabisa huu ni wakati wako wewe mfanya biashara

+255758061575 & +255684860817

henrylameck@gmail.com

henrylameck90@yahoo.com

Tukuyu Tour & Safari

Vadacom Ni Zaidi

Tembelea g2g.fm upate movie Kali

Tembelea g2g.fm upate movie Kali

Kilimo Kwanza

Hlm servise

Latest movie

Movies

Computer books

Computer books